Rais Kikwete ziarani Marekani, Canada


Rais Jakaya Mrisho Kikwete

Na Mwandishi wetu

Rais Jakaya Kikwete ameanza rasmi ziara ya kikazi nchini Marekani na ya kiserikali nchini Canada.

 

Rais Kikwete na ujumbe wake aliondoka nchini juzi na aliwasili katika  jiji la New York, Marekani jana, tayari kwa ziara hizo.

 

Atakuwa Marekani kwa siku mbili kabla ya kwenda Canada kwa ziara rasmi ya kiserikali ya siku mbili.

 

Katika ziara yake mjini New York, Rais Kikwete leo atakutana na kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon ofisini kwa Katibu Mkuu huyo wa UN.

 

Baada ya mazungumzo hayo, Rais Kikwete ataungana na Ban Ki Moon, Meya wa Jiji la New York na mfadhili mkubwa wa misaada ya kibinadamu duniani, Michael Bloomberg; Mama Helen Agerup ambaye ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Misaada ya Kibinadamu ya H&B Agerup na Dk. Kelly Henning, Mkurugenzi wa Mipango ya Sekta ya Afya ya Taasisi ya Bloomberg Philanthropies kwenye uzinduzi wa matokeo ya Mpango wa Ubunifu wa Afya ya Akinamama Tanzania.

 

Kwenye sherehe hiyo iliyopangwa kufanyika kwenye ukumbi wa Green kwenye makao makuu ya UN, Rais Kikwete, Ban Ki Moon, Bloomberg na mama Helen Agerup kwa pamoja watazindua matokeo ya mpango huu uitwao Innovative Maternal Health Program.

 

Kwenye shughuli hiyo pia Meya Bloomberg atatangaza matokeo ya miaka mitatu ya misaada ya kiafya chini ya mpango huo kwa akinamama iliyotolewa na taasisi ya inayomilikiwa na Meya Bloomberg ya Bloomberg Philanthropies.

 

Aidha, kwenye shughuli hiyo, Meya Bloomberg pia atatangaza msaada mpya wa mabilioni ya fedha kuboresha afya ya akinamama Tanzania chini ya mpango huo na atatangaza mshirika mpya ambaye atasaidiana na taasisi ya Bloomberg Philanthropies katika kuunga mkono huduma bora za afya kwa akinamama wa Tanzania.

 

Misaada ya taasisi ya Bloomberg Philanthropies huelekezwa katika maeneo ya vijijini yasiyokuwa na huduma bora zaidi za kiafya na huduma ambazo hutolewa ni zile za kuokoa maisha ya akina mama hasa wakati wa uzazi.

Post a Comment

0 Comments