Sheikh amwagiwa tindikali

  Ni Katibu wa Mufti Zanzibar

 Na Mwinyi Sadallah


Rais Jakaya Kikwete akimjulia hali Katibu wa Mufti wa Zanzibar, Sheikh Fadhili Soraga jana.

Katibu wa Mufti Zanzibar, Sheikh Fadhir Suleiman Soraga, amemwagiwa tindikali na watu wasiyojulikana huko Magogoni Msumbiji Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar jana.

Akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya Jeshi la Polisi Ziwani Zanzibar, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai,Yussuf Ilembo, alisema Sheikh Soraga alimwagiwa tindikali majira ya alfajiri alipokuwa akifanya mazoezi ya viungo.

Ilembo alisema wakati akifanya mazoezi, alimuona mtu akifanya mazoezi akielekea mbele yake na baada ya kukutana uso kwa uso alimmwagia tindikali na kumjeruhi sehemu za usoni na kifua kabla ya mtu huyo kutoweka.

“Tumepokea taarifa za kusikitisha na za kinyama za kumwagiwa tindikali kwa Katibu wa Mufti… mtu mwenye akili hawezi kufanya kitendo cha kinyama kama hicho,” alisema.

Alisema tayari uchunguzi umeanza kufanyika na Jeshi la Polisi litahakikisha linatumia nguvu zake zote kuwasaka watu waliohusika na mpango wa hujuma dhidi ya kiongozi huyo.

“Tayari tumeanza kufanya uchunguzi mkali dhidi ya watu waliohusika na mpango wa kumhujumu Sheikh Soraga,” alisema.

Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Rufaa ya Manazi Mmoja, Dk. Jamala Adam Taib, alisema Sheikh Soraga, amejeruhiwa usoni na kifuani na kulazimika kusafirishwa kwenda katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MHN) jijini Dar es Salaam kwa matibabu.

Hata hivyo, alisema ni mapema kueleza Sheikh Soraga ameathirika kwa kiwango gani baada ya kumwagiwa tindikali hadi hapo uchunguzi wa kitibabu utakapokamilika.

“Ni mapema kusema ameathirika kwa kiwango gani kabla ya kukamilika kwa uchunguzi wa kitibabu,” alisema Dk. Jamala.

Baada ya kuteremshwa katika gari la wagonjwa Toyota DFP 5049, Sheikh Soraga alipakiwa katika ndege ya serikali yenye namba 5H-TGF Tanzania, saa 3:45 asubuhi kupelekwa Dar es Salaam na kusidikizwa na viongozi mbalimbali wa serikali akiwamo Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali iddi.

KAULI YA MUFTI

Akizungumza na waandishi wa habari katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Zanzibar, Mufti wa Zanzibar, Sheikh Saleh Kabi, aliwataka Waislamu na wananchi kuwa na subira kufuatia tukio hilo.

Mufti Kabi alisema katika mafundisho ya Mwenyezi Mungu, binadamu ametakiwa kuwa na uadilifu katika maisha yake ya kila siku ikiwamo kulinda heshima yake na viongozi wake.

Alisema Zanzibar inaweza kuingia katika maafa makubwa iwapo watu tawakosa uadilifu utavunjika kidogo na kuwataka wananchi kurudi katika mafundisho ya mwenyezi muugu ikiwemo kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuvuruga amani na umoja wa kitaifa.

Alisema wakati umefika kwa viongozi wa dini wafanye kazi ya dini na viongozi wa siasa wafanye kazi ya siasa badala ya kuchanganya.

Mufti Kabi alisema matatizo yalioikuba Rwanda na kusababisha maelfu ya raia wake kupoteza maisha yalitokana na kutozingatiwa kwa mgawanyo wa majukumu baina ya viongozi wa kisiasa na dini.

CCM YALAANI

Wakati huo huo; Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimeshauri serikali kuomba msaada wa uchunguzi kutoka mashirika ya kimataifa kufutia matukio ya vitendo vya uhujuma dhidi ya raia na mali zao Zanzibar.

Ushauri huo umetolewa Katibu Mwenezi wa CCM Zanzibar, Issa Haji Gavu, katika taarifa yake kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana baada ya tukio la kuwa Soraga kumwagiwa tindikali.

“Kama Jeshi la Polisi uwezo wake mdogo wa kuwafichua waharifu hawa, basi ni vyema wakaomba msaada kwenye vyombo vya upelelezi vya kimataifa kama vile Interpol,” alisema Gavu.

Alisema yapo mashirika ya upelelezi ya kimataifa yenye uwezo mkubwa wa uchunguzi wa mitandao ya makundi ya uharifu na kama watafanyakazi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi, vitendo vya hujuma dhidi ya raia na mali zao vitadhibitiwa kwa muda mwafaka Zanzibar.

CUF: NI UNYAMA

Chama cha Wananchi (CUF) kimewataka wananchi wa Zanzibar kushirikiana na Jeshi la Polisi kuwafichua watu waliohusika na kitendo hicho.

Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Salim Bimani, alisema katika taarifa yake kuwa : “Tunawaomba wananchi watimie mashirikiano kwa kuwafichua wale wote wanaotenda uovu Zanzibar.”

Aidha, alisema vyombo vya dola likiwamo Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina ili waliohusika na uhujuma dhidi ya kiongozi huyo wachukuliwe hatua ili sheria ichukue mkondo wake.

“Chama cha wananchi CUF kina waomba wanachama wake, wananchi wote kwa jumla kutojiingiza katika vitendo viovu vinavyoashiria uvunjifu wa amani nchini,” alisema Bimani.

“Tendo la uovu lililofanywa dhidi ya Sheikh Soraga limeleta huzuni na simanzi kubwa kwa wananchi wa Zanzibar,” alisema Bimani.

MAMIA WAFURIKA HOSPITALI

Mamia ya wananchi jana walifurika katika hospitali ya Mnazi Mmoja baada ya kupokea taarifa za kiongozi huyo maarufu Zanzibar kuwa amemwagiwa tindikali na watu wasiojulikana visiwani humo.

Baadhi ya wananchi walishindwa kujizuia na kulazimika kutokwa na machonzi baada ya kuona uso wa Sheikh Soraga ulivyoathiriwa na tindikali.

Katika Hospitali ya Mnazi Mmoja baadhi ya wagonjwa waliokuwa wamelazwa walilazimika kuacha vitanda na kuanza kuchungulia wakiwa gholofani wakifuatilia tukio la kingozi huyo.

Tukio la kumwagiwa tindikali Sheikh Soraga limetanguliwa na matukio ya makanisa 25 na baa 12 kuchomwa moto Zanzibar katika kipindi cha mwaka mmoja.

JK AMJULIA HALI MUHIMBILI

Rais Jakaya Mrisho Kikwete jana alikwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kumjulia Sheikh Soraga katika chumba cha uangalizi maalumu (ICU) Muhimbili ambako amelazwa kwa matibabu muda mfupi baada ya kuwasili kutoka visiwani Zanzibar.

Kikwete alitembelea Sheik huyo hospitalini hapo baada ya kuwasili jijini Dar es Salaam akitoka katika ziara ya kikazi katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Manyara na Singida baada ya kupata taarifa kuwa amejeruhiwa kwa kumwagiwa tindikali na watu wasiojulikana wakati akifanya mazoezi.

Rais Kikwete amemtakia Sheikh Soraga kupata nafuu ya haraka ya majeraha aliyopata kutokana na tukio hilo.

Post a Comment

0 Comments