Mia tano ya CHUMA (Sarafu) yaja!




Benki Kuu la Tanzania (BoT) lipo kwenye mkakati mzito wa kutengeneza sarafu ya sh 500 badala ya noti kwa kuwa ipo kwenye mzunguko mkubwa.

 

Akiongea kwenye mahojiano na kituo kimoja cha Radio cha jijini Dsm, Gavana wa BoT, Profesa Benno Ndullu, alisema mzunguko wa noti ya sh 10,000 si mkubwa hivyo inaishi umri mrefu zaidi kuliko noti ya sh 500, hali inayosababisha uchakavu wa noti hizo na kuilazimu BoT kuchapisha nyingine.

 

“Mzunguko wa noti ya sh 10,000 si mkubwa kama wa sh 500… kwa hiyo fedha zote zikitoka sisi tunatarajia zitarudi kupitia mabenki, tunaangalia zile zilizobaki na hali nzuri, zile ambazo si nzuri tunabadilisha tunatoa nyingine.

 

“Lakini kuweza kukaa moja moja haiwezekani hakuna noti inayoweza kukaa daima dumu, hakuna… hili ni tatizo mojawapo lililo kubwa kwa noti tunazoita denomination (thamani) ya chini sasa tunalitafutia ufumbuzi.

 

“Kipindi cha nyuma sh 500 ilikuwa pesa nyingi na mzunguko wake haukuwa wa haraka kama ilivyo sasa, solution (ufumbuzi) yake si noti tu hata coin (sarafu) ya sh 500 tuiangalie pia,” alisema Gavana Ndullu.

Post a Comment

0 Comments