Askari watano JWTZ wajeruhiwa katika ajali, mmoja afariki


Na Elizabeth Zaya

Watu wawili wamefariki dunia papo hapo, akiwamo askari wa Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Koplo William Mwaikambo, na wengine sita kujeruhiwa kufuatia gari la jeshi hilo kugongana uso kwa uso na gari la kiraia aina ya Toyota Coaster.

Koplo Mwaikambo alikuwa ni dereva wa gari la Makao Makuu ya JWTZ.

Tukio hilo lilitokea jana jijini Dar es Salaam, eneo la Kwa Warioba, Mikocheni, wakati gari la jeshi likitokea makao makuu ya jeshi likirudisha walinzi Lugalo.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na makao makuu ya JWTZ ilieleza kuwa daladala lililokuwa likiendeshwa na Musa Hamad Rajabu lililipita gari aina ya DCM na kuhamia upande wa pili wa barabara na kisha kugongana uso kwa uso na gari la jeshi.

Taarifa hiyo imewataja waliojeruhiwa kuwa ni Luteni Kileo, Praveti Charles Mwamnyanyi, Praveti Godbless Manyanga, Koplo Fred Nkamata na Praveti Shimoti Nicademus, wote wa JWTZ, pamoja na raia, Mohamed Omari.

Wote wamelazwa katika Hospitali ya Lugalo na taratibu za mazishi ya askari aliyefariki zinaandaliwa.

Post a Comment

0 Comments