*NI BAADA YA KUVAMIA MAANDAMANO YAO,WENZAO IRINGA WAANGUA VILIO MKUTANONI
Waandishi Wetu
WAZIRI
wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi jana alionja shubiri ya
hasira za waandishi wa habari, baada ya kutimuliwa kwenye maandamano yao
waliyoyafanya Dar es Salaam kulaani mauaji ya mwenzao Daudi Mwangosi.
Maandamano
hayo yaliyoanzia katika Kituo cha Televisheni cha Channel Ten,
yamefanyika ikiwa zimepita siku 10 tangu kuuawa kwa Mwangosi ambaye
alikuwa mwandishi wa kituo hicho, mkoani Iringa.
Mwangosi aliuawa
kwa bomu la machozi wakati polisi walipokuwa wakiwadhibiti wafuasi wa
Chadema waliokuwa katika sherehe za kuzindua tawi lao katika Kijiji cha
Nyololo, Iringa, Septemba 2, mwaka huu.
Dk Nchimbi alifukuzwa na
kuzomewa muda mfupi baada ya maandamano hayo kufika katika Viwanja vya
Jangwani ambako yalihitimishwa kwa matamko mbalimbali.
Waziri huyo
alifika kwenye viwanja hivyo sambamba na maandamano hayo na kusimama
pembeni karibu na eneo ambalo waandishi walikuwa wakikusanyika.
Baada
ya viongozi wa maandamano hayo kupita kuelekea mbele, Dk Nchimbi
aliungana nao jambo lililopokewa kwa hisia tofauti na idadi kubwa ya
wanahabari hao ambao walianza kuhoji ujio wake, lakini kikubwa wakitaka
aondolewe.
“Umekuja kufanya nini, kwani sisi tulikualika?” alisikika akisema mmoja wa waandishi hao. Baada
ya swali hilo, Waziri Nchimbi aliomba apewe risala iliyoandaliwa na
waandishi hao, lakini kinyume chake alijibiwa kuwa risala ni mabango
yaliyokuwa na ujumbe wa kulaani mauaji hayo, hivyo na kumtaka ayasome
kwa umakini.
Baadhi ya mabango hayo yalisomeka: “Tunaomba mamlaka
kuunda tume huru ya uchunguzi wa mauaji ya Daudi Mwangosi....
Tunasikitika na tunalaani mauaji ya mwandishi wetu mkoani Iringa.”
Mabango
mengine yalisomeka: “Mwema (IGP) unangoja nini?, Kalamu na kamera zetu
ni zaidi ya risasi na mabomu yao, polisi wawajibike, damu ya Mwangosi
isafishe Jeshi la Polisi.
Mengine yaliyosomeka: “Polisi wamemuua
Mwangosi,Hatunyamazi kwa mtutu wa bunduki.... Mtatuua lakini tutaandika
ukweli, Why killing the messenger? [Kwa nini mnamuua mjumbe?] na polisi
kutuua basi.
Wakati waandishi wakipiga kelele kutaka waziri huyo
aondoke, aliendelea kuwapo eneo hilo, huku akitabasamu na kujaribu
kuomba kuzungumza.
Kitendo hicho kiliwafanya waandishi kuanza
kumzomea, huku wakimtaka aondoke eneo hilo kwa kuwa hakualikwa na
maandamano hayo yalipaswa kuhutubiwa na waandishi wenyewe kupitia kwa
viongozi wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF).
Huku akiwa haamini
kinachoendelea na mzozo huo kutimia dakika saba, mwandishi wa habari
mwandamizi, Nyaronyo Kicheere alikwenda kupaza sauti akimwambia
kinagaubaga waziri huyo kwamba mkutano huo haumhusu wala kiongozi yeyote
wa Serikali.
“Haya ni maandamano ya waandishi wa habari,
hatukumwalika kiongozi yeyote wa siasa au Serikali,” alisema Nyaronyo
huku akishangiliwa na waandishi wenzake.
Mbali na kupiga kelele za
kumtaka Waziri Nchimbi aondoke, waandishi hao walikuwa wakiimba nyimbo
mbalimbali za mshikamano, sambamba na kuonyesha picha za marehemu
Mwangosi.
Mwishowe, Waziri Nchimbi aliyekuwa amevalia kaunda suti
ya rangi ya maziwa, aliamua kuondoka kwa unyonge, huku akisindikizwa kwa
kelele za kumzomea.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya
kuondolewa eneo hilo, Waziri Nchimbi alisema Serikali inawathamini
waandishi wa habari na itaendelea kushirikiana nao.
“Kupitia fursa
hii naomba niwaagize makamanda wa polisi wa mikoa kuandaa mikutano na
waandishi wa habari ili kujenga mazingira mazuri ya kufanya kazi, kwa
maana hatuwezi kuendelea katika hali kama hii,” alisema Waziri Nchimbi.
Matukio mengine Maandamano
hayo pia yaliambatana na matukio mengine kadhaa ikiwamo waandishi
kulala barabarani, huku wengine wakiigiza kuua kwa mtutu wa bunduki.
Uliibuka
pia mjadala wa wanahabari hao kutumia moja ya magari yaliyokuwa
yakisindikiza maandamano hayo kama jukwaa. Hoja hiyo ilipingwa na
wazungumzaji wote kulazimika kutumia kifusi cha mchanga uliokusanywa
katika eneo hilo.
Waandishi zaidi ya 100 walikutana katika Kituo
cha Channel Ten katikati ya jiji la Dar es Salaam na kuanza maandamano
hayo saa 2:48 asubuhi. Walifika Jangwani saa 3:30.
Mbali na
waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali nchini, maandamano hayo pia
yaliwashirikisha wanafunzi wa vyuo vya uandishi wa habari kikiwamo cha
Dar es Salaam, (DSJ) ambao nao walikuwa na bango lenye ujumbe wa kulaani
mauaji hayo.
Vilio, Simanzi vyatawala Iringa Vilio
na simanzi jana vilitawala viunga vya bustani ya Manispaa ya Iringa
ambako waandishi wa habari walihitimishia maandamano yao ya amani
yaliyoandaliwa kulaani kuuawa kwa mwenzao, Mwangosi.
Machi 6,
mwaka huu marehemu Mwangosi alisimama katika bustani hiyo na kutoa tamko
la waandishi wa habari kupinga manyanyaso, ubaguzi na vitisho kwao
kutoka baadhi ya taasisi za Serikali ikiwamo polisi.
Maandamano
hayo yaliyovuta hisia za wadau wa kada mbalimbali wakiwamo wanaharakati
wa haki za binadamu, yalianzia katika Ofisi za Chama cha Waandishi wa
Habari Mkoa wa Iringa (IPC) saa 4:15 asubuhi.
Karibu muda wote wa
maandamano hayo, waandishi hao walikuwa wakilia kiasi cha kuwafanya hata
baadhi ya wananchi waliowashuhudia wakipita katika mitaa kadhaa ya
Manispaa ya Iringa nao kububujikwa na machozi.
Mratibu wa
maandamano hayo, Zulfa Shomari alisema hicho ni kielelezo na ishara ya
kulaani ukatili uliofanywa dhidi ya mwandishi huyo akiwa anatekeleza
majukumu yake.
“Sisi wanahabari Mkoa wa Iringa tunaungana na
wenzetu nchini kulaani vikali mauaji yaliyofanywa na Jeshi la Polisi
dhidi ya Mwangosi ambaye alikuwa akitekeleza wajibu wake wakati Chadema
wakiendesha shughuli zao za ndani za kichama,” alisema Shomari.
Alisema
licha ya tukio hilo, wataendelea na msimamo wao wa kutoshirikiana na
polisi mpaka kamati iliyoundwa itakapotoa taarifa zenye ukweli na
kuridhisha kuhusu mauaji hayo ikiwa ni pamoja na watuhumiwa kufikishwa
mahakamani.
“Nashangaa kuona Serikali inapoteza kodi za wananchi
kuchunguza mauaji yaliyofanywa na polisi wakati suala liko wazi ikiwamo
ushahidi wa picha zilizopigwa wakati mauaji hayo yakitekelezwa,”
alisema.
Katibu wa kamati ya maandamano hayo, Daniel Mbega alisema
anashangaa kuona Jeshi la Polisi linawashambulia wanahabari wakati
wanasaidia kufichua mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa
umma.
“Ninashangaa sana kuona polisi wanaua raia wasiokuwa na
hatia kwa kutumia silaha badala ya kuwalinda, utafikiri nchi yetu iko
katika vita ya wenyewe kwa wenyewe! Tunachohitaji kufahamu kamera na
Laptop ya Mwangosi viko wapi ?” alihoji Mbega.
Imeandikwa na Fidelis Butahe, Aidan Mhando, Ibrahim Yamola, Geofrey Nyang’oro Dar; Frederick Siwale na Clement Sanga, Iringa
0 Comments