Ujenzi wa Daraja la Kigamboni waanza

UJENZI: DARAJA KIGAMBONI Daraja la Kigamboni likiendelea kujengwa katika Bahari ya Hindi, eneo la Kurasini, Dar es Salaam jana. Daraja hilo linatarajiwa kuwa na njia sita litakapokamilika na hivyo kuwa daraja kubwa zaidi katika Afrika Mashariki na Kati. Picha na Aron Msigwa




Na George Njogopa                                                                       

UJENZI wa Daraja la Kigamboni jijini Dar es Salaam, umeanza kwa kishindo na jana Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli alitembelea eneo hilo na kuwahimiza makandarasi kukamilisha kazi hiyo kwa muda uliopangwa.


Daraja hilo linalojengwa na Serikali kwa kushirikiana na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), linatarajiwa kukamilika katika kipindi cha miaka mitatu huku likigharimu Sh214 bilioni.


Ujenzi wa daraja hilo unafanywa na Kampuni ya China Railways Construction na China Major Bridge Engineering Company, zote za nchini China.


Akizungumza na makandarasi hao, Waziri Magufuli aliwataka waongeze kasi ya ujenzi na kuahidi kwamba Serikali itatoa ushirikiano wa hali na mali ili kukamilisha kazi hiyo.


"Nataka niwahakikishie kwamba Serikali itaendelea kuwa bega kwa bega nanyi. Lakini najua nyie ni wachapa kazi, mnaweza kufanya kazi usiku na mchana na kufanya ujenzi uchukue miezi 30 badala ya 36 ya sasa," alisema Dk Magufuli.


Waziri Magufuli pia alitumia fursa hiyo kuwaonya wataalamu hao juu ya kile alichokiita kuendesha ujenzi wa kiwango cha chini.


"Hapa lazima niwe mkweli kwamba Serikali haitasita kuchukua hatua kali, iwapo ujenzi huu utafanywa katika hali ya kulipua. Tunataka ubora, tena ubora unaoeleweka," alisisitiza.


Waziri Magufuli ambaye katika ziara hiyo aliambatana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,  Said Meck Sadiq alieleza kufurahishwa na kasi ya ujenzi huo na kuwataka wamalize kazi kwa wakati kwa kuwa Serikali haitaongeza muda.

Post a Comment

0 Comments