
Katibu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (Tef), Neville Meena
Waandishi wetu
WAANDISHI wa habari wa mikoa mbalimbali nchini, leo
wanatimiza azma yao ya kufanya maandamano ya amani ya kimyakimya nchi
nzima kulaani kuuawa kwa mwenzao, Daud Mwangosi katika tukio lililotokea
Septemba 2, mwaka huu.Mwangosi aliuawa kwa kitu kinachodhaniwa kuwa ni
bomu la machozi wakati polisi walipokuwa wakiwadhibiti wafuasi wa
Chadema waliokuwa katika uzinduzi wa tawi lao katika Kijiji cha Nyololo,
Iringa.
Katika Mkoa wa Dar es Salaam, maandamano hayo yataanzia
katika Kituo cha Televisheni cha Channel Ten na kuishia katika Viwanja
vya Jangwani.
Katibu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (Tef),
Neville Meena alisema jana kuwa maandamano hayo yataanza saa 2:00
asubuhi yakiwashirikisha waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari.
Awali,
maandamano hayo yalipangwa kuanzia Channel Ten, Mtaa wa Jamhuri na
kupita katika Mtaa wa Azikiwe, Barabara ya Bibi Titi hadi katika Viwanja
vya Mnazi Mmoja. Kuhusu hilo, Meena alisema mabadiliko hayo yamefikiwa
katika mkutano baina ya viongozi wa Tef na polisi.
Alisema
mkutano huo ulitokana na uamuzi wa jeshi hilo wa jana asubuhi kuyapiga
marufuku maandamano kwa madai kwamba hayakufuata taratibu.
Kamanda
wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema
maandamano hayo yalikuwa yamezuiwa na Polisi Mkoa wa Ilala baada ya
kuona taratibu zilikiukwa.
Hata hivyo, kamanda huyo alisema baadaye
alilazimika kuitisha kikao na wawakilishi wa wanahabari hao na
kukubaliana kuhusu mabadiliko hayo ya ratiba.
Mrakibu Mwandamizi
wa Polisi Mkoa wa Ilala, Lazaro Mambosasa alidai kuwa yalikuwa yamezuiwa
kutokana na barua kuchelewa kuwafikia. Barua hiyo ilifikishwa katika
ofisi hizo Jumamosi.
Alisema ombi la ulinzi kwenye maandamano
linapaswa kufika polisi kabla ya saa 48 ili lifanyiwe kazi, kanuni
ambayo jukwaa hilo lilikuwa limekiuka.
“Tulisikia taarifa ya
kuwepo kwa maandamano katika vyombo vya habari wakati kibali cha ombi la
maandamano hayo bado hakijafika kwetu,” alidai Mambosasa. “Tulishangaa
kufuatwa asubuhi na mmoja wa viongozi wa Tef kufuatilia kibali chao cha
maandamano juu ya kupatiwa ulinzi wa askari. Lakini hadi tunaonana naye
tulikuwa bado hatujapata barua yoyote ya kuomba kibali hicho.”
Juzi,
Kaimu Mwenyekiti wa Tef, Theophil Makunga alisema waandishi
watakaoshiriki maandamano hayo watavaa ama nguo nyeusi au watafunga
vitambaa vyeusi mkononi ikiwa ni ishara ya kuomboleza na kulaani kuuawa
kwa mwenzao.
Makunga alisema uamuzi wa kufanyika kwa maandamano hayo
ulifikiwa katika kikao cha Jukwaa hilo kilichofanyika Jumamosi, Dar es
Salaam.
Ziara ya JK yazuia maandamano Arusha
Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa
Arusha, Claud Gwandu alisema Polisi imewazuia kufanya maandamano hayo kwa kisingizio cha ziara ya Rais Jakaya Kikwete.
Gwandu
alisema maandamano yao ni ya amani na kwamba hayajapangwa kufika eneo
ambalo Rais au mkutano wake utafanyika.“Tunakutana kujadiliana lakini
polisi wamezuia wakitaka tupange siku nyingine kwa vile anasema askari
wengi wa ulinzi watakuwa katika mkutano wa Rais na ziara yake,” alisema
Gwandu.
Mikoa mingine
Mkurugenzi wa Umoja wa Klabu za
Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), Abubakar Karsani alisema maandalizi
katika klabu mbalimbali mikoani yamekamilika isipokuwa Ruvuma.
Alisema katika mkoa huo, UTPC imeagiza kusitishwa kwa maandamano hayo ili kupisha maandamano ya Chadema.
“Tumewaagiza
waandishi kusitisha maandamano yao kupisha maandamano ya Chadema, kwani
hatuwezi kuyachanganya na yale ya vyama vya siasa, hivyo wao
wataandamana siku nyingine,” alisema.
Alisema tofauti na Mkoa wa
Ruvuma, Mkoa wa Rukwa polisi ilizuia waandishi kuandamana kwa madai
kwamba taarifa ilipaswa kutolewa saa 48 kabla ya kuandamana.
Mwenyekiti
wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga, Shija Felician
alisema maandalizi ya mkutano huo yamekamilika.Alisema waandishi wa
Zanzibar walikuwa katika maandalizi kwa ajili ya kufanikisha maandamano
hayo.
Polisi wahaha
Katika hatua nyingine, askari wanne kati ya watano waliokamatwa kwa tuhuma za mauaji hayo wameachiwa huru.
Habari
zilizolifikia gazeti hili jana zimeeleza kuwa kuachiwa kwa askari hao
kumekwenda sambamba na polisi kufanya jitihada za kumnusuru mtuhumiwa
aliyebaki ambaye anakabiliwa na kesi ya mauaji.
Habari hizo zimeeleza
kuwa, baada ya kukamatwa Jumatatu na kuhojiwa kwa siku tatu, askari hao
waliachiwa na kuruhusiwa kurudi mikoani kwao.
“Walihojiwa na
baadaye kuruhusiwa kurudi, lakini yule aliyeonekana kumlipua mwandishi
huyo kwa bomu ambaye ameonekana kwenye vyombo mbalimbali vya habari
anaendelea kushikiliwa,” kilidokeza chanzo cha habari ndani ya polisi.
Mmoja
wa watuhumiwa hao walioachiwa alisema anamshukuru Mungu kwa kusikiliza
kilio chake hata akaachiwa na kuruhusiwa kurejea kwenye kituo chake cha
kazi.
Alipoulizwa nini kinaendelea kwa mwenzao aliyebaki alijibu:
“Ninachojua ameitwa mwanasheria wetu wa (polisi) kuangalia uwezekano wa
kuifanya kesi hiyo iwe ya man slaughter (kuua bila kukusudia) badala ya
murder (kuua kwa kukusudia). Ila alitakiwa kufikishwa mahakamani leo.”
Kamati
iliyoundwa na Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi kuchunguza
kifo cha mwandishi huyo, jana ilikutana na waziri huyo kupata maelekezo
ya awali.
Dk Nchimbi aliunda kamati hiyo inayoongozwa na Jaji Stephen
Ihema na kuipa hadidu sita za rejea katika utekelezaji wa majukumu
yake.
Tendwa: Polisi walikosea kuizuia Chadema Iringa
Msajili
wa Vyama vya Siasa, John Tendwa amesema polisi walifanya makosa
kukiruhusu CCM kufanya kampeni katika Jimbo la Bububu, Zanzibar na
kukizuia Chadema, kufanya ufunguzi wa matawi yake Iringa.
Mbali na
hilo, Tendwa alisema ataibadili sheria ya utoaji vibali vya kufanya
mikutano ya vyama vya siasa kutoka polisi na kutolewa na ofisi yake
ikiwa wadau watapendekeza hivyo na Bunge kuridhia mabadiliko hayo.
Tendwa
alitoa kauli hiyo Dar es Salaam mwishoni mwa wiki alipokuwa akichangia
mada kuhusu ‘ongezeko la mauaji katika mikutano ya siasa ni kukua kwa
demokrasia?’ katika kituo cha Televisheni cha ITV.
Msajili huyo alisema sheria hiyo inaweza kubadilishwa na kumpa mamlaka ya kutoa vibali, endapo wadau watakuwa na kauli moja.
“Unakuta
chama kinaomba kufanya mkutano wiki mbili kabla, lakini majibu
hayatolewi kwa wakati kitendo ambacho kinasababisha kurudisha nyuma
demokrasia.”
Alisema polisi ni moja na haitakiwi kujichanganya
katika utoaji wake uamuzi. Alisema CCM iliruhusiwa kufungua kampeni zake
Bububu na Chadema kuzuiwa kuandamana kwa kile kilichodaiwa kuwa Sensa
ya Watu na Makazi ilikuwa ikiendelea, jambo alilosema ni makosa kwa kuwa
kilichokuwa kikifanyika bara (sensa) na visiwani kilikuwa kikiendelea.
Hata
hivyo, Tendwa alisema kuwa mara baada ya mauaji kutokea maeneo tofauti
nchini kumekuwapo na matamko mbalimbali yanayotolewa na watu na taasisi
bila kuwapo hitimisho lake, hivyo ameandaa mjadala kuangalia eneo lenye
makosa katika demokrasia ya Tanzania.Mwanasheria wa Kituo cha Sheria na
Haki za Binadamu (LHRC), Harold Sungusia alisema polisi imekuwa
ikisababisha mauaji ya wananchi wasio na hatia.
Sungusia alisema
mfumo wa polisi umepitwa na wakati na kinachotakiwa hivi sasa ni
kufanyika kwa mabadiliko ya kuwaandaa askari hao ili wawatumikie
wananchi na si kuwaua.SPC yataka RPC
Iringa akamatwe
Kwa
upande wake, Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga (SPC),
kimeiomba Serikali kuchukua hatua za haraka kumkamata Kamanda wa Polisi
Mkoa wa Iringa Michael Kamuhanda na kumuunganisha na polisi wenzake
kwenye mauaji ya kinyama ya Mwangosi.
Felician alisema
yaliyofanyika jana mjini Kahama amedai kama Serikali ilimkamata Abdallah
Zombe ambaye Cheo chake ni sawa na Kamuhanda kwa nini yeye asikamatwe
ambapo kosa lake lina ushahidi wa kutosha kwamba alihusika kwa namna
nyingine.
Mwaka 2007 Serikali ilimkamata aliyekuwa Mkuu wa
Upelelezi wa makosa ya Jinai mkoani Dare Es Salaam, Zombe baada ya
vijana wake kufanya mauaji ya wafanyabiashara watatu kwa maagizo yake
lakini baadaye aliaachiwa na mahakama kosa ambalo halikuwa na ushahidi
wa kutosha tofauti na la RPC Kamuhanda ambaye Mwandishi aliuawa yeye
akishuhudia.
Mwenyekiti huyo alisema anashangaa Serikali kutumia
gharama ya kuunda tume huku wauaji wakiongozwa na RPC huyo wanafahamika
kwenye picha mbalimbali wanaonekana ambapo kwenye kesi ya Zombe
aliyekamatwa na kufikishwa mahakamani hakuna picha iliyoonekana polisi
wakiua wafanyabiashara hao.
Alisema RPC Kamuhanda hawezi kukwepa
kwamba hakuhusika na Mauaji hayo kutokana na mashuhuda mbalimbali
waliokuwepo kwenye eneo la tukio ambao wengi wao walidai walithubutu
hata kumfuata kwenye gari lake wakimtaka awazuie polisi wake wasimuue
mwandishi huyo lakini ilidaiwa alipandisha kioo cha gari na kufunga
kabisa na kuashiria kwamba hakuwa tayari kumsaidia mwandishi huyo
asiuawe.
Felician alisema ili Watanzania wajue haki imetendeka
vizuri bila kuonea polisi wadogo, RPC naye akamatwe na kuunganishwa kama
mmoja wa watuhumiwa kwa mauaji hayo kwa kuwa polisi wadogo hupokea amri
kutoka kwa wakubwa na wameua mbele yake hivyo naye anahusika .
Septemba
2, mwaka huu tasnia ya habari ilipata pigo kubwa kwa kuuawa mwandishi
wa habari na wanaodhaniwa kuwa ni polisi waliokuwa wakidhibiti mkutano
wa CHADEMA mkoani Iringa hali ambayo imebeba uzito mkubwa kwa nguvu
kubwa iliyotumika na polisi kwa kumdhibiti mwandishi mmoja wa habari
ambaye silaha yake ni kamera na kalamu.
Katika mauaji hayo
askari watano walikamatwa na leo chama hicho cha waandishi wa Habari
Mkoa wa Shinyanga kitafanya maandamano makubwa ya amani kulaani mauaji
hayo na kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Umoja wa Vilabu vya waandishi wa
Habari Tanzania, Abubakari Karsani maandamano hayo yatafanyika nchi
nzima.
_
Imeandikwa na Frederick Katulanda, Aziza Masoud, Pamela Chilongola, Zaina Malongo na Ibrahim Yamola.
0 Comments