Kova: Tunachunguza utapeli wa mke wa kigogo wa Polisi



Raymond Kaminyoge

KAMANDA wa Kanda Maalum ya Polisi  Mkoa wa Dar es Salaam, Suleiman Kova amesema jeshi la Polisi linalifanyia kazi tuhuma za utapeli unaomhusisha mke wa kigogo wa jeshi hilo na kwamba leo litatoa taarifa.

Mbali na tukio hilo, jeshi hilo litatoa taarifa za uchunguzi za majambazi yaliyopora mamilioni ya fedha kwenye  Benki ya Commercial Bank of Afrika (CBA) lililotokea Alhamisi iliyopita.

Kamanda Kova alisema jana jijini Dar es Salaam alipozungumza na Mwananchi kwa simu baada ya kutakiwa kuzungumzia matukio hayo.

“Ninayafanyia kazi mambo mliyoyaandika leo kwenye Mwananchi, nitatoa taarifa kesho pamoja na upelelezi wa majambazi yaliyoiba mamilioni ya fedha katika benki ya CBA unavyoendelea,” alisema Kova.

Alisema masuala yote hayo atayatoa kwenye mkutano na waandishi wa habari unaotarajia kufanyika leo.

Jana, gazeti hili liliandika habari za watu 120 wenye elimu ya chuo kikuu waliodai kutapeliwa mke wa mmoja wa makamishna wa jeshi la Polisi waliopo makao makuu kwa kuchangishwa zaidi ya Sh100 milioni.

Walichangishwa fedha hizo kwa ajili ya kufanyiwa mpango wa kupata ajira katika Idara ya Usalama wa Taifa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) lakini baadaye ilikuja kubainika kwamba ulikuwa utapeli.

(Toka Gazeti la Mwananchi)

Post a Comment

0 Comments