Dk Nchimbi aunda kamati kuchunguza kifo cha Mwangosi

Dk. Emmanuel Nchimbi Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi


Waandishi Wetu

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi ameunda kamati ya watu watano kuchunguza mauaji ya Mwandishi wa Habari wa Kituo cha Channel Ten, Daudi Mwangosi. Akitangaza kamati hiyo Dar es Salaam jana, Dk Nchimbi aliwataja wajumbe wake kuwa ni Jaji Mstaafu, Steven Ihema ambaye atakuwa Mwenyekiti na Mwakilishi wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Theophil Makunga.


Wajumbe wengine ni Mwakilishi wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Pili Mtambalike, Mtaalamu wa milipuko kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kanali Wema Wapo na Naibu Kamishna wa Polisi (DCP), Isaya Mngulu. Mwangosi alifariki Septemba 2, mwaka huu baada ya kupigwa na kitu kinachosadikiwa kuwa ni bomu wakati polisi walipokuwa wakiwadhibiti wafuasi wa Chadema. “Kamati hii nataka inipe majibu ndani ya siku 30 na kama utaalamu utakuwa hautoshi tutaomba msaada nje,” alisema Dk Nchimbi.


Alisema kamati hiyo itasaidia kujibu maswali sita ambayo hivi sasa hayana majibu kutokana na tukio hilo. “Tuna maswali sita ambayo mimi sina majibu yake. Swali la kwanza tunataka kujua nini chanzo cha kifo cha Daudi? Pili tujue ni kweli kwamba kuna uhasama kati ya polisi na waandishi Iringa?” alisema Dk Nchimbi na kuongeza: “Tatu tujue kama ni kweli kuna orodha ya waandishi watatu wa kushughulikiwa Iringa? Nne kama nguvu zilizotumika zilistahili? Tano kama kuna utaratibu wa vyama vya siasa kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa polisi? Mwisho kujua uhusiano wa Jeshi la Polisi na vyama vya siasa ukoje?”


Dk Nchimbi alisema, sheria lazima zifuatwe kwani nchi ikiingia kwenye matatizo, Serikali haitaweza kuwaeleza wananchi kwamba ndicho kitu kinachotakiwa... “Hatutaki tuwe na vita vya wenyewe kwa wenyewe.”


Katika hatua nyingine, Waziri Nchimbi alisema anashangazwa na kutohojiwa kwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kutokana na ujumbe aliomtumia Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Said Mwema siku moja kabla ya tukio.

 Chadema wamwangukia JK     Chadema kimemwomba Rais Jakaya Kikwete kuwasimamisha kazi Mkurugenzi wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Kamishna Paul Chagonja, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Michael Kamuhanda pamoja na askari saba walioshiriki kwenye vitendo vya mauaji ya Mwangosi ili kupisha uchunguzi wa kina kuhusu tukio hilo.


Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema,  John Mnyika alisema kuwasimamisha kazi viongozi hao kutasaidia kufanyika kwa uchunguzi wa haki, jambo ambalo linaweza kurudisha imani ya wananchi kwa Serikali yao. “Ni tukio la kinyama kwelikweli ambalo limeitia doa Serikali, ili waweze kujisafisha, tunamwomba Rais Kikwete kutumia mamlaka aliyonayo kwa kuwachukulia hatua kali wahusika, jambo ambalo linaweza kurudisha imani kwa wananchi,” alisema Mnyika.


Alisema kuwajibika kwao kutasaidia kupata taarifa sahihi kuhusu kifo hicho kwa sababu wataweza kumtambua kiongozi aliyewatuma askari hao kufanya mauaji hayo ili aweze kuchukuliwa hatua.


Chama cha Wananchi (CUF) kimelitupia lawama Jeshi la Polisi kuwa limehusika na vurugu zilizotokea Iringa na kusababisha kifo cha Mwangosi.


Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa CUF,  Profesa Ibrahim Lipumba alisema, Jeshi hilo linastahili kubeba lawama za vurugu na kifo cha mwandishi huyo kwa kuwa lilishindwa kuheshimu makubaliano yaliyofikiwa baina yao na Chadema.


“Kwa mtazamo huu, CUF tunaona wanaopaswa kubeba lawama hii ni Jeshi la Polisi na wala si (Chadema), kwani kama tulivyoeleza awali, ilitosha kuheshimu makubaliano yaliyofanyika baina yao na hata kama kulitokea vurugu haikuhitajika kutumika nguvu kubwa kiasi hiki,” alisema Profesa  Lipumba.


Tucta Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta) limeitaka polisi kubuni mbinu mpya za kisasa katika matumizi ya silaha wakati wa kukabiliana na vurugu zinazotokana na harakati za kisiasa.


Akitoa tamko hilo Dar es Salaam jana, Kaimu Katibu Mkuu wa Tucta, Hezron Kaaya alisema kama kweli mauaji hayo ya mwanahabari yamefanywa na askari polisi, jeshi hilo linaipeleka nchi pabaya.


“Ikumbukwe kuwa matukio yanayoonekana madogo leo ndiyo ambayo baadaye huzaa machafuko makubwa katika nchi. Haya tumeyashuhudia katika nchi nyingine na kamwe Tucta hatupendi nchi yetu ifike huko. Tunalaani mauaji hayo na tutapenda kuona uchunguzi wa kina na ulio huru unafanyika na taarifa kamili ya tukio hilo itolewe kwa umma,” alisema Kaaya.


Habari hii imeandikwa na Boniface Meena, Zaina Malongo, Patricia Kimelemeta, Geofrey Nyang'oro na Magreth Munisi.

Post a Comment

0 Comments